UKWELI MCHUNGU:WASOMI WETU HAWANA SOKO KIMATAIFA


Najua kauli yangu hii itawakera wengi hususan hao wanaojiita wasomi, lakini najua kwamba ukweli mara nyingi huwa unauma sana.

Katika orodha ya nchi za Afrika ambazo wasomi wake wanaibwa na kusombwa na kupelekwa huko Ulaya na Marekani kufanya kazi , Tanzania haitajwi kabisa.

Watanzania wengi wanaokwenda nje kufanya kazi, ni vibarua zaidi, wenyewe wanajiita wabeba mabox, na hata kama ni wasomi, basi utawakuta wanafanya kazi ambazo huwezi kusema zitaweza kuisaidia nchi.

Hata hivyo wapo Watanzania wachache sana ambao wamenunuliwa nje na kufanya kazi huko kwa sababu ya uwezo wao kiufahamu katika taaluma zao.

Lakini hii yote ni kutokana na mfumo wetu wa elimu ambao kwa miaka mingi umekuwa ukidumaza akili zetu.
Mara nyingi wadau mbalimbali wakiwemo baadhi ya wanasiasa wamekuwa wakipiga kelele kuhusu haja ya Serikali kubadili mfumo wa elimu ili kuweza kuwashindanisha wasomi wake na wasomi wa nchi nyingine duniani lakini jambo hilo limeonekana kama vile halina maana.

Najua serikali kupitia wizara ya elimu na mafunzo ya ufundi stadi imeshawahi kubadili mitaala ya elimu mara kdhaa, lakini ninachojaribu kusema hapa ni je tabia ya wanafunzi kukariri ili wafaulu mitihani badala ya kuelewa imekomeshwa kwa kutafuta chanzo chake?

Ukweli ni kwamba, ni vigumu kwa wasomi wengi wa Tanzania kushindana kwenye soko la dunia kitaaluma kwa sababu, hawakuandaliwa kuwa watu wanaofahamu, bali wameandaliwa kuwa watu wanaokariri…

0 comments: